Thursday, January 18, 2018

Bunduki ya kivita yenye skafu ya Chadema yakamatwa Shinyanga


Kamanda wa polisi mkoa wa Shinyanga ACP Simon Haule akionesha silaha aina ya AK-47 yenye namba 18116428 na mafuta ya kulainishia silaha yaliyotupwa na majambazi waliotaka kuvamia kiwanda cha Jielong 
 Jeshi la polisi mkoa wa Shinyanga limefanikiwa kukamata silaha ya kivita aina ya AK-47 iliyotupwa na watu wanaodaiwa kuwa ni majambazi waliokuwa wanataka kuvamia kiwanda cha kutengeneza mafuta ya kupikia cha Jielong Holdings (Tanzania) Ltd kilichopo Nhelegani katika kata ya Kizumbi manispaa ya Shinyanga.

Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari leo Alhamis Januari 18,2018 Kamanda wa polisi mkoa wa Shinyanga ACP Simon Haule amesema walikamata silaha hiyo usiku wa kuamkia leo majira ya saa tano eneo la Tinde wakati majambazi hao wanafuatiliwa na polisi ndipo wakaamua kutupa bunduki hiyo.

“Silaha hii aina ya AK-47 yenye namba 18116428 ilikuwa imefungwa kwenye skafu yenye rangi ya nembo ya Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) ikiwa na risasi 25 ndani ya magazine yake na risasi zingine 8,zikiwa kwenye mfuko mdogo wa nailoni”,alieleza Kamanda Haule.

“Majambazi wawili pia walitelekeza pikipiki aina ya SANLG yenye namba za usajili MC 856 BPF,mafuta ya cherehani ya kulainishia silaha,tochi mbili na koti zito”,aliongeza.

Alisema jeshi la polisi lilipata taarifa za majambazi hao kutaka kuvamia kiwanda hicho kinachomilikiwa na raia wa China tangu tarehe 6.01.2018 kisha kuanza kuwafuatilia na kubaini kuwa baadhi yao ni wakazi wa Kahama na Ushirombo ambapo amewataka kujisalimisha polisi.

    Choose :
  • OR
  • To comment
No comments:
Write comments