Monday, January 22, 2018

Sugu afikishwa kizimbani Leo


Mbeya. Mbunge wa Mbeya Mjini (Chadema), Joseph Mbilinyi ‘Sugu’  amefikishwa mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya leo Januari 22, 2018 kusikiliza kesi inayomkabili  ya kutumia lugha ya fedheha dhidi ya Rais John Magufuli.

Sugu pamoja  Katibu wa Chadema Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Emmanuel Masonga walifikishwa mahakamani hapo Januari 19, 2018 lakini  mahakama ilizuia dhamana zao na kuwarejesha rumande hadi leo.

Siku hiyo hakimu mkazi mfawidhi wa mahakama hiyo, Michael Mteite alitoa uamuzi wa kuwarejesha rumande, kwamba kesi hiyo inatakiwa isikilizwe mfululizo kwa muda mfupi na washtakiwa wakiwa wanafika mahakamani hapo wakitokea mahabusu.

“Mahakama hii inataka kusikiliza kesi hii kwa muda mfupi sana, ndani ya wiki moja kuanzia Jumatatu ijayo (leo)  iwe imeamuriwa, hivyo washtakiwa wataendelea kuwekwa mahabusu,” amesema Mteite.

Sugu na Masonga wameshtakiwa kwa kosa la kutumia lugha ya fedheha dhidi ya Rais John Magufuli ambayo waliyatoa katika mkutano wa hadhara walioufanya Desemba30 mwaka jana wakiwa viwanja vya Shule ya Msingi Mwenge jijini Mbeya

    Choose :
  • OR
  • To comment
No comments:
Write comments