Wednesday, January 24, 2018

Walichokibaini Polisi Baada ya Kumhoji ‘Nabii’ Tito





JESHI la Polisi mkoani Dodoma,  baada ya kumkamata na kumfanyia mahojiano Onesmo Machija (44) anayejiita ‘nabii’ Tito, kutokana na mahubiri ya kidini anayoyafanya, limesema mtu huyo ana  matatizo ya akili.

Akizungumza na wanahabari mjini Dodoma leo, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Dodoma, Gillesi Muroto, amesema mnamo Juni 23, 2014, mtu huyo aliwahi kulazwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa ajili ya matibabu ya akili chini ya daktari aliyejulikana kwa jina moja la William ambapo aliporuhusiwa alitakiwa kurejea hospitalini hapo Julai 9 mwaka huohuo lakini hakurejea.

Kamanda Muroto aliendelea kusema kwamba baada ya hapo, Machija ambaye kanisa lake halijasajiliwa popote,  aliibukia mkoani Dodoma katika kijiji cha Nong’ona kilicho karibu na Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom) akifanya  mahubiri ya kidini yaliyodaiwa kuwa hayakuwa na maadili ya kidini.

Kwa msingi huo, alisema jeshi la polisi limempeleka Hospitali ya Rufaa ya Mirembe iliyoko mkoani Dodoma  kwa ajili ya kumpima tena matatizo hayo ya akili na baada ya majibu kutolewa,  Dkt. Dixon Philipo aliyemshughulikia alithibitisha kwamba bado ana matatizo hayo.

Pamoja na hayo, Muroto alisema jeshi la polisi mkoani humo  bado linaendelea kumshikilia kutokana na matendo yake aliyoyafanya ili kufanya uchunguzi zaidi



    Choose :
  • OR
  • To comment
No comments:
Write comments